Ujenzi wa hospitali ya Rufaa Kanda ya Chato wamkosha Rais Nyusi

0
176

Rais Filipe Nyusi wa Msumbiji aliyeanza ziara yake hii leo nchini, ameweka jiwe la msingi katika ujenzi wa hospitali ya Rufaa Kanda ya Chato.

Akizungumza baada ya Rais Nyusi kuweka jiwe hilo la msingi, Rais Dkt John Magufuli amesema kuwa, atahakikisha ujenzi wa hospitali hiyo unakamilika haraka.

Amesema hospitali hiyo itakayokuwa na uwezo wa kuhudumia zaidi ya watu milioni 15 , itahudumia watu kutoka maeneo mbalimbali.

Ameziagiza Mamlaka zinazohusika na ujenzi huo kuhakikisha awamu zote za ujenzi zinafanyika kwa mara moja na si kuchukua muda mrefu.

Kwa upande wake Rais Nyusi ameipongeza Serikali ya awamu ya tano chini ya Dkt Magufuli kwa kuwajali Wananchi wake hasa katika huduma za afya.

Amesema kitendo cha Serikali kujenga hospitali kubwa Chato ni cha kuigwa, sababu hospitali hiyo itahudumia watu wengi kutoka ndani na nje ya nchi.

Rais Nyusi amesema ataendelea kumkumbusha Rais Magufuli kila mara kuhusu kukamilika kwa hospitali hiyo, lengo likiwa ni kutaka ikamilike haraka.