Rais Magufuli akerwa TAKUKURU kutaka kujenga ofisi Chato

0
404
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli alipokuwa akizungumza mara baada ya kumuapisha Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mbunge wa Iramba Magharibi) kuwa Waziri wa Katiba na Sheria. Hafla imefanyika Wilayani Chato Mkoani Geita, Mei 3, 2020.

Rais John Magufuli ameelezwa kukerwa na kitendo cha Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Tanzania (TAKUKURU) kuomba feddha kiasi cha shilingi bilioni 1 za kujenga ofisi wilayani Chato mkoani Geita wakati tayari wana ofisi.

“Mmesema hapa mnataka kujenga ofisi ya TAKUKURU wilayani Chato, lakini tulishawapa jengo tena la ghorofa. Msizungumze mambo kwa kunifurahisha mimi, mjipendekeze Chato wakati nimeshaondoka kwenye Urais,” ameeleza Rais Magufuli.

Rais Magufuli amesema hayo katika hafla ya kuzindua majengo saba ya taasisi hiyo jijini Dodoma ambapo pia ameeleza kutoridhishwa na gharama zilizotumika kuyajenga kwa sababu ni kubwa sana.

Amesema kuwa tayari moyo wake umekuwa sugu hivyo hawezi kufurahishwa na mtu anayezungumzia Chato kwa sababu yeye si mbinafsi. Akitilia mkazo katika hilo ameiagiza taasisi hiyo kumchunguza mtumishi aliyependekeza ijengwe ofisi nyingine Chato wakati tayari kuna ofisi na kwamba kitendo hicho kinaweza kuwa na dalili za rushwa.

Mbali na kuipingoza taasisi hiyo kwa kazi kubwa inayofanya kukabiliana na rushwa nchini, lakini amesema ina mapungufu ikiwa ni pamoja na kushindwa kuwachukulia hatua stahiki watumishi wake wanaotenda vitendo vya rushwa pamoja na kuchelewesha kupelekea kesi za rushwa mahakamanio.

Akizungumzia gharama za nyumba hizo alizozizindua leo, amesema ni kubwa sana ikilinganishwa na hali halisi ya nyumba zenyewe, lakini ameamua kuzizindua kwa heshima kutokana na kazi kubwa ambayo TAKUKURU wamekuwa wakifanya.

Katika hatua nyingine ameahidi kutoa shilingi bilioni 2 kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za watumishi wa TAKUKURU jijini Dodoma, na ameagiza Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) lipewe tenda ya kujenga nyumba hizo mara baada ya eneo la kujenga litakapopatikana.

Ameiasa taasisi hiyo kuendelea kukabiliana na vitendo vya rushwa hasa kipindi hiki cha uchaguzi mkuu ili kuhakikisha wananchi wanapata viongozi wanaowataka na sio wale wanaotwaa madaraka kwa kutumia nguvu ya fedha zao.