Kesi ya Mbowe kushambuliwa yakosa ushahidi wa kutosha

0
295

Jeshi la polisi limesema kuwa limekosa ushahidi wa kuonesha kuwa Freeman Mbowe alishambuliwa kwani mbali na Mbowe na dereva wake mashahidi wengine waliohojiwa wameshindwa kuthibitisha kutokea kwa tukio hilo.

Msemaji wa Jeshi la Polisi, David Misime katika taarifa kwa vyombo vya habari amesema “Kwa mujibu wa mashahidi hawa hakuna hata mmoja aliyeweza kusikia kelele hizo au kuona mbowe akishambuliwa. Kwa mantikini hiyo ushahidi pekee unaozumngumzia kushambuliwa ni maelezo ya mhanga wa tukio(Mbowe) pamoja na dereva wake.”

Aidha, polisi wamesema kuwa Mbowe alikuwa amelewa chakari siku aliposhambuliwa baada ya kutembelea sehemu kadhaa za starehe ikiwemo ‘Royal Village.’

“Hata hivyo alipofika hospitali alionekana akiwa katika hali ya ulevi chakari kiasi cha kushindwa kutamka maneno sawa sawa. Tunaendelea na uchunguzi kutafuta ukweli wa tukio hili, hivyo tunaomba wananchi wenye taarifa zinazoweza kusaidia upelelezi huo wazilete kwetu. Tutaendelea kutoa taarifa kwenu kadri ushahidi utakavyopatikana,” ilieleza taarifa hiyo.