KIGOMA: Serikali kuwafikisha mahakamani wakimbizi

0
282

Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi ameviagiza vyombo vya ulinzi na usalama mkoani Kigoma kuwaondosha na kuwafungulia mashtaka wakimbizi zaidi ya 1,000 waliotoroka kutoka katika kambi mbalimbali na kwenda kufanya uhalifu nje ya kambi.

Mhandisi Hamad Masauni ameyasema hayo wakati akiongea na wakimbizi kutoka nchini Burundi katika Kambi ya Nduta iliyoko wilayani Kibondo, kambi yenye jumla ya wakimbizi na waomba hifadhi 75,055.

Aidha, Masauni amewataka wakimbizi kuendelea kujiandikisha kwa hiari ili waweze kurudi nchini mwao, Burundi, ambako hali ya amani sasa imerejea na tayari pande tatu ikiwemo Tanzania, Burundi, na Shirika la Kuhudumia Wakimbizi Duniani (UNHCR) zimetia saini mkataba utakaofanikisha zoezi hilo kwa wanaotaka kurejea.

Akizungumza katika mkutano huo Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Kibondo, Kanali Hosea Ndagala amesema wao kama Kamati ya Ulinzi na Usalama watahakikisha kila atakayethibitika kufanya uhalifu sheria itachukua mkondo wake ikiwemo kufutiwa ukimbizi na kufunguliwa mashtaka.