Joto la pambano la Wilder na Fury lazidi kupanda

0
486

Mabondia Deontay Wilder na Tyson Fury wamekutana uso kwa uso ikiwa ni siku mbili kabla ya pambanao lao litakalofanyika Februari 22 kwenye ukumbi wa MGM Grand mjini Las Vegas nchini Marekani na kuonyeshana ubabe huku kila mmoja akijigamba kumlambisha mwenzie sakafu.

Katika kile kinachoonekana  kuonyeshana ubabe uliopitiliza, Wilder amesema alimsaidia Fury kuondoka katika dimbwi la matumizi ya dawa za kulevya na kumrejesha katika ulimwengu wa masumbwi kauli ambayo Fury ameipinga kwa kumwambia Wilder kuwa kama si yeye pengine asingakaa apande kwenye ulingo wa MGM Grand na yeye ndiye mtu pekee aliyemfanya kupokea malipo ya juu zaidi katika mchezo wa ngumi.

Fury alirejea kwenye ulingo kwa kupamabana na Wilder mwezi Disemba mwaka 2018 ikiwa ni miezi sita tangu aliporejea katika mchezo huo, kufuatia kukaa nje kwa miezi 30 kutokana na matumizi ya dawa za kulevya na pombe kupita kiasi vitendo vilivyomsababishia matatizo ya kiafya.

Katika pambano lao la mwisho mwezi Disemba mwaka 2018 walitoka sare na kila mmoja hakuridhika na matokeo hayo na sasa ulimwengu wa masumbwi unasubiri kuona nani mbabe wa kweli kati yaDeontay Wilder na Tyson Fury katika pambano lao la Februari 22.