Uamuzi wa Malkia wa Uingereza kuhusu Prince Harry na Meghan kujiuzulu

0
408

Kufuatia kikao cha familia ya kifalme ya Uingereza kilichofanyika leo Jumatatu, Januari 13, 2020, Malkia wa Uingereza, Elizabeth II amesema familia imeridhia uamuzi wa mjukuu wake, Prince Harry na mkewe Meghan kujitoa katika nyadhifa za kifalme na kuishi kwa kujitegemea wenyewe.

Malkia Elizabeth amesema kuwa familia ilitamani wanandoa hao wabaki katika majukumu yao ya kifalme, lakini wameelewa na wanaheshimu uamuzi wao wa kuanza maisha yao mapya ya kujitegemea.

Harry na Meghan wametanabaisha kuwa hawatotegemea fedha za umma katika maisha yao mapya wanayoyaanza, badala yake watakuwa wakijitegemea kiuchumi.

Pamoja na familia kukubali kusudio lao imesema kutakuwa na kipindi cha mpito ambapo wanandoa hao watakuwa wakiishi Canada na Uingereza.

Hata hivyo, Malkia Elizabeth amesema hayo ni masuala ya kifamilia ambayo ni magumu sana kuamua, na bado kazi kubwa inahitajika kufanyika, na ameomba uamuzi wa mwisho ufikiwe katika siku zijazo